Macho ya dunia ya soka yataelekezwa katika Uwanja wa New York/New Jersey nchini Marekani usiku wa leo majira ya saa 7 wakati mabingwa mara tano wa dunia Brazil watakapokutana na Morocco katika mchezo wa Kundi C wa Kombe la Dunia 2026.
Pambano hili linatajwa kuwa moja ya mechi kubwa zaidi za hatua ya makundi kutokana na kukutanisha timu mbili zinazoshika nafasi za juu duniani na ambazo zina ndoto za kufika mbali kwenye mashindano hayo.
Brazil enzi mpya chini ya Ancelotti
Brazil inaingia kwenye michuano hii ikiwa chini ya kocha mpya Carlo Ancelotti, ambaye amepewa jukumu la kuirejesha timu hiyo kileleni baada ya miaka kadhaa ya kushindwa kufika hatua za mwisho za Kombe la Dunia. Selecao bado inatafuta taji lake la sita la dunia, huku mara ya mwisho kulitwaa ikiwa mwaka 2002.
Nguvu kubwa ya Brazil ipo kwenye safu yake ya ushambuliaji inayojumuisha nyota kama Vinicius Junior, Raphinha na Endrick. Hata hivyo, taarifa za hivi karibuni zinaeleza kuwa Neymar hatakuwa sehemu ya mchezo huu kutokana na majeraha.
Morocco sio timu ya kubeza
Kwa upande wa Morocco, Atlas Lions wanaingia kwenye mchezo huu wakiwa na kumbukumbu nzuri ya kufika nusu fainali ya Kombe la Dunia 2022 na kuandika historia kama taifa la kwanza kutoka Afrika kufika hatua hiyo. Tangu hapo wameendelea kuimarika na sasa wanatajwa kuwa miongoni mwa timu hatari zaidi duniani.
Morocco itamtegemea nahodha wake, Achraf Hakimi, pamoja na kiungo mkabaji Sofyan Amrabat na mshambuliaji Brahim Diaz. Uwezo wao wa kucheza kwa nidhamu ya hali ya juu na kufanya mashambulizi ya kushtukiza ndiyo silaha inayowafanya kuwa tishio kwa timu yoyote.
Vita ya mbinu
Mchezo huu unatarajiwa kuwa vita ya mbinu kati ya timu inayopenda kumiliki mpira dhidi ya timu inayojua kujilinda na kushambulia kwa kasi.
Brazil itatafuta kutumia kasi ya Vinicius Junior na ubunifu wa viungo wake kutoboa ukuta wa Morocco. Kwa upande mwingine, Morocco itajaribu kuwabana Wabrazil katikati ya uwanja na kutumia nafasi za mashambulizi ya kushtukiza kupitia Hakimi na Brahim Diaz.
Historia inasemaje?
Hii itakuwa mara ya pili kwa mataifa haya kukutana kwenye Kombe la Dunia. Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 1998 ambapo Brazil ilishinda mabao 3-0 kupitia Ronaldo, Rivaldo na Bebeto. Hata hivyo, Morocco ya sasa ni tofauti kabisa na ile ya miaka hiyo, jambo linalofanya mchezo huu kuwa mgumu kutabirika.
Nani ana nafasi kubwa?
Kwa ubora wa kikosi na uzoefu wa mashindano makubwa, Brazil wanaingia kama timu tishio huku Morocco wakiwa uder-dog. Hata hivyo, rekodi ya Morocco ya kusumbua vigogo wa dunia inaonyesha kuwa Selecao hawatakuwa na kazi rahisi.
Utabiri
Brazil 2-1 Morocco
Brazil wanaonekana kuwa na ubora kidogo kwenye maeneo muhimu ya ushambuliaji, lakini Morocco wana uwezo wa kufanya mchezo huu kuwa mgumu hadi dakika za mwisho.
Mashabiki wa soka duniani wanatarajia kushuhudia moja ya mechi bora zaidi za hatua ya makundi ya Kombe la Dunia 2026.



